News
Mtambo wa Kisasa
Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Profesa Shukrani Manya amefanya ziara katika Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na kufanya kikao kazi pamoja na uongozi na watumishi wote.
Katika kikao hicho, Naibu Waziri amewataka wafanyakazi kufanya kazi kwa uadilifu na kutumia karama, talanta na taaluma walizonazo katika utendaji kazi wao ili kuifanya STAMICO kuwa na manufaa kwa umma.
Amesema kila mtumishi anayefanya kazi kwa uadilifu matokeo ya kazi yake yanaonekana hivyo ni vyema kuweka jitihada katika kuleta matokeo chanya na kuweka maslahi ya Taifa mbele.
Ameitaka STAMICO kuongeza kasi katika kufanya mazungumzo na wadau wake hususan wawekezaji wabia ili kuhakikisha wanafikia muafaka katika uendeshaji wa miradi mbalimbali ili iweze kuanza uzalishaji na hasa Mgodi wa Dhahabu wa Buckreef ulioko mkoani Geita.
“Lengo letu ni kuona miradi yenu inaanza uzalishaji ili iweze kuchangia katika Pato la Taifa, tumieni rasilimali mlizonazo katika kuwekeza maeneo yenye tija ili kuweza kujiongezea faida”.