Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

State Mining Corporation

State Mining Corporation

News

MITAMBO ILIYOZINDULIWA NA RAIS DKT. SAMIA YAANZA KAZI YA KUCHORONGA KWA WACHIMBAJI WADOGO-NYAMONGO .


Kwa mara ya kwanza Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limefanya uchorongaji katika maeneo ya Wachimbaji wadogo kwa kutumia Mitambo ya Uchorongaji maalum kwa Wachimbaji Wadogo iliyozinduliwa na Rais Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan mwishoni mwa mwezi Oktoba 2023.

Uchorongaji huu umefanyika kwa mara kwanza Disemba 4, 2023 ambapo Mgeni Rasmi Meja Jenerali (Mstaafu) Michael Isamuhyo Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugezi ya STAMICO, Viongozi na Wachimbaji Wadogo wameshuhudia mitambo hiyo ikichoronga na kutoa sampuli kutoka umbali wa mita 100 chini ya ardhi katika Kijiji cha Kerende -Nyamongo Wilayani Tarime.

Akizungumza katika Tukio hilo Mej. Jen. ( Mstaafu) Isamuhyo amesema uzinduzi wa Mitambo hii ni Mwendelezo wa Maagizo ya Rais wa Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan tukio lilofanyika 21 Oktoba 2023 Dodoma wakati wa hafla ya uzinduzi wa vifaa kwa ajili ya Wachimbaji Wadogo.

Isamuhyo amesema kwamba Serikali kupitia STAMICO wamepanga kununua jumla ya mitambo 15 kwa ajili ya Wachimbaji Wadogo na kwa sasa mitambo ambayo imeshafika 5 na huu ni mmoja wa Mtambo hiyo mitano.

Mitambo hii itakuwa msaada mkubwa kwa Wachimbaji na itawasaidia Wachimbaji kujua taarifa ya kijiolojoa katika maeneo yao ya uchimbaji kwa hiyo watachimba kwa tija.

Awali akitoa salamu toka Kamati ya Kudumu ya Bunge Nishati na Madini Makamu Mwenyekiti Mhe. Kilumbe Shabani ameipongeza STAMICO kwa kuwezesha Mitambo hiyo kufika kwa Wakati kwa Wachimbaji Wadogo mara tu baada ya Kuzinduliwa na Mhe. Rais Dodoma. Na Serikali itatoa kipaumbele kwa sekta ya Madini hasa Wachimbaji Wadogo katika kuwapatia nishati ya Umeme katika Maeneo yao ya Migodi ya Uchimbaji.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse amesema katika kuhakikisha Mitambo hii inaleta tija kwa Wachimbaji Wadogo, Shirika imeigawanya Mitambo hii ya awali kikanda kwa kuzingatia kiwango cha Shughuli za Uchimbaji mdogo nchini.

Amesema katika eneo hilo la Kerende Wataalum wa Shirika wamefanya utafiti wa awali katika maeneo mbalimbali ya Wachimbaji ambapo hadi sasa jumla ya Wachimbaji wanane wamefikiwa na wanne kati yao wameonesha nia ya kutaka huduma ya Uchorongaji.

Mbunge wa Tarime Vijijini Mhe. Mwita Waitara akitoa neno katika Uzinduzi huo alisema Mgodi wa Barrick tayari umeyatambua maeneo kwa ajili ya kuwalipa fidia wachimbaji wadogo na kuwaomba kuharakisha ulipaji huo wa fidia kwa Wachimbaji Wadogo kwa kuchelewa kuwalipa kwa Wakati kuna sababisha Migogoro kwa Wachimbaji hao.

Kwa upande wa wachimbaji wadogo, ndugu Stephen Jumanne Kwa niaba ya rais wa FEMATA ameishukuru STAMICO kwa kuleta mitambo hii kwa ajili ya Wasaidia Wachimbaji Wadogo na Sasa Watakuwa Wanachimba madini kwa uhakika bila kubahatisha ukilinganisha na awali ambapo walikuwa wanapoteza fedha nyingi katika uchimbaji husiokuwa wa uhakika.

Aidha tukio hili limeshuhudiwa Kamati ya Bunge Nishati na Madini, Mkurugenzi Mtendaji STAMICO, Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Mbunge wa Tarime Vijijini, FEMATA na Tawoma ambapo Uchorongaji huo umeanzia rasmi kwa Mmoja wa Wachimbaji wadogo Rajabu Mining Aliyepata Kerende-Nyamongo Wilayani Tarime.