STAMICO YASHIRIKI JUKWAA LA WAKUU WA MASHIRIKA NA TAASISI AFRICA
Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), lilichukua nafasi kubwa katika Kongamano la Wakurugenzi Watendaji wa Mashirika na Taasisi wa Afrika lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kigali kuanzia tarehe 14 hadi 15 Mei 2026, likitoa fursa kubwa za madini kwa zaidi ya viongozi 2,800 wa biashara duniani, watunga sera na Wawekezaji wa kimataifa.
Huku ujumbe wa viongozi wa Tanzania uliohudhuria Kongamano hilo ukiongozwa na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angela Jasmine Kairuki.
Akizungumza na wawekezaji Mhe. Kairuki alisema kuwa, Tanzania ina fursa ya kimuundo na kisheria kwa ajili ya ushirikiano wa kimkakati. "Tanzania sio tu chaguo la uwekezaji, lakini chaguo bora zaidi barani Afrika," alisema.
Kando ya Kongamano hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Dk. Venance Mwasse alifanya mazungumzo na wawakilishi wa kampuni kubwa ya madini ya Rio Tinto kujadili uwezekano wa ubia wa leseni zinazomilikiwa na STAMICO.
Dk. Mwasse pia alikutana na Mwenyekiti wa Amsons Group, Bw. Edha Nahdi kujadili ushirikiano wa kimkakati katika uchimbaji wa dhahabu na fursa ya kutumia Makaa ya mawe ya STAMICO yenye ubora wa hali ya juu.
Zaidi ya hayo, mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Biashara ya Tanzania, Adam Mihayo yalilenga katika kupata masuluhisho ya kifedha kwa Wachimbaji Wadogo.
Msukumo mkali wa STAMICO kwa washirika wa kimkakati unawiana na lengo kuu la nchi la kujenga uchumi wa dola trilioni 1 chini ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050.