RAFIKI BRIQUETTES YA STAMICO RASMI KUTUMIKA CHUO CHA MAFUNZO ZANZIBAR
Shirika la Madini la Taifa ( STAMICO) katika muendelezo wa kuhakikisha linaendelea kuwa kinara katika kuhamasisha matumizi ya Nishati safi Tanzania nzima, leo tarehe 11/8/2026 limeingia mkataba wa pande tatu na Chuo cha Mafunzo Zanzibar na Taasisi ya Foundation for Disabilities Hope ( FDH ) ya kuhakikisha vyuo vyote vya mafunzo ( Magereza) Zanzibar vinaanza kutumia Nishati safi ya kupikia ya Rafiki Briquettes.
Makubaliano hayo yamefanyika katika ukumbi wa Chuo cha Mafunzo Zanzibar na kushuhudiwa na Kamishna wa Magereza Zanzibar Khamis Abdalah Khamis, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse na Mkurugenzi wa FDH Bwn. Michael Salali.
Akiongea katika hafla hiyo, Dkt. Mwasse ameipongeza Taasisi ya FDH kwa kufanikisha kuingia makubaliano haya ambayo yatawezesha vyuo vyote vya Mafunzo (Magereza) Zanzibar kupata Nishati hii ya Rafiki Briquettes ambayo inaenda kuleta afueni kwenye gharama za Nishati ya kupikia kwa vyuo hivyo lakini pia kuanza kutekeleza agenda ya Nishati safi kwa Taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100.
Dkt. Mwasse pia ameahidi kusaidia kuleta mafunzo na Kongamano la kuhamasisha matumizi ya Nishati safi kwa Watumishi wa vyuo hivyo vya Mafunzo (Magereza) na Wananchi wote wa Zanzibar.
Awali akiongea na kutoa salamu kutoka FDH, Bwn. Salali ameahidi kushirikiana na STAMICO kuhakikisha Nishati hii inafika kwenye vyuo vyote vya Mafunzo (Magereza) kwa wingi na inafika katika ubora unaostahili.
Naye, Kamishna Khamis ameishukuru na kuipongeza STAMICO kwa kuhakikisha Nishati hii inafika Zanzibar.
Ameomba pia STAMICO iangalie namna ya kuwapa fursa hii ya kusambaza Nishati hii kwa wale wafungwa ambao wamemaliza vifungo vyao ili iwe njia ya kujitengenezea kipato baada ya kumaliza vifungo vyao.
Kamishna ameahidi kutoa ushirikiano kwa STAMICO na FDH katika kuhakikisha Nishati hii inatumika katika Magereza yote ya Zanzibar kutekeleza agenda ya kuhakikisha taasisi zote zinazohudumia zaidi ya watu 100 zinatumia Nishati safi katika matumizi yake ya kila siku.
STAMICO imejipanga kuhakikisha inaendelea kuwa kinara katika kuhamasisha matumizi ya Nishati safi ya kupikia Tanzania nzima.